- Pinda Amfukuzia (atoshana nguvu na Zitto)
- Wengine wasindikiza kwa mbali
- Umaarufu wa CCM waongezeka kiduchu
WAKATI baadhi ya wanasiasa wakiwa wameanza kujiwinda kwa ajili
ya kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015, Shirika la Utafiti la
Synovate limetoa matokeo ya utafiti wake ambao unaonyesha vigogo tisa
kuwamo katika mchuano huo.
Utafiti huo umeonyesha kuwa endapo uchaguzi
huo ungefanyika sasa, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema), Dk Willibrod Slaa angeibuka mshindi baada ya kuongoza orodha
hiyo akipata asilimia 17.
|
Dr.Wilbrod Slaa |
Katika matokeo ya utafiti huo uliofanywa
Desemba mwaka jana, Dk Slaa anafuatiwa kwa mbali na Waziri Mkuu, Mizengo
Pinda ambaye amefungana na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe
kila mmoja akipata asilimia tisa.
Hata hivyo, licha ya kuongoza, Dk Slaa
ameporomoka kwa asilimia 25 ikilinganishwa na matokeo ya utafiti kama
huo uliofanywa na taasisi hiyo mwaka 2011 ambapo alipata asilimia 42.
Kadhalika, umaarufu wa Pinda ambaye anaongoza
miongoni mwa wagombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), umeshuka kwa
asilimia tatu kutoka 12 za mwaka juzi, wakati Zitto ameendelea na
kiwango kilekile cha asilimia tisa alizopata katika utafiti
uliotangulia.
Wengine wanaofuata na asilimia walizopata kwenye mabano
ni Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli (8), Waziri Mkuu wa zamani,
Edward Lowassa (7) na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba (5).
Pia wamo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano
wa Kimataifa, Bernard Membe (4) ambaye amefungana na Mwenyekiti wa
Chadema, Freeman Mbowe (4) na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Samuel Sitta (2).
Ikilinganishwa na utafiti wa 2011, Lipumba ameporomoka kwa asilimia tisa.
Lowassa
amepanda kwa asilimia sita, Dk Magufuli asilimia nne, Mbowe na Membe
wamepanda kwa asilimia mbili kila mmoja, wakati Sitta amebaki katika
kiwango kilekile cha asilimia mbili.
Hata hivyo, utafiti huo umeonyesha kuwa
wananchi ambao hawana uamuzi wa kuchagua mtu yeyote kati ya hao kwa sasa
ni asilimia 18, likiwa ni ongezeko la asilimia 12 ikilinganishwa na
utafiti uliotangulia.
CCM yatamba
Katika utafiti huo, CCM
kimeonyesha kuwa ni chama ambacho asilimia 52 ya wananchi wangependa
kujiunga nacho, kikiwa kimepanda chati kwa asilimia moja kutoka asilimia
51 mwaka jana.
Kwa upande wa Chadema, wananchi ambao wanapenda kujiunga nacho imeshuka kutoka asilimia 35 mwaka 2011 hadi 31 mwaka jana.
Uwezekano mkubwa wa CCM kupanda chati ni
kutokana na ukweli kuwa mwaka jana kilikuwa na uchaguzi ulioanzia ngazi
ya mashina hadi taifa na kuibua vuguvugu kubwa masikioni mwa wananchi.
Chadema hakikuwa na harakati kubwa za kisiasa
ukiacha kampeni ya Movement For Change (M4C), ambayo kwa kiasi haikuwa
na pilika kama uchaguzi wa CCM.
Chama kingine ni CUF ambacho kimeporomoka kwa kupata asilimia 10 mwaka 2011 hadi nne mwaka 2012.
Hata hivyo, asilimia ya wananchi kutokutaka
kujihusisha na chama chochote imepanda kutoka asilimia mbili mwaka 2011
hadi 12 mwaka 2012.
Source:
www.mwananchi.co.tz