Sunday, April 14, 2013

Aliyenyonga wanawe 2, kuua mke kizimbani


MKAZI wa kijiji cha Majimoto wilayani Mlele katika mkoa wa Katavi, Justine Albert (24) amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Mpanda akikabiliwa na makosa matatu ya mauaji.
 
Albert, juzi alifikishwa mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Kiganga Tegwa akishitakiwa kuwaua kwa kuwanyonga watoto wake wawili, Frank Justine (6) na Eliza Justine (4) huku miili yao akiitumbukizwa kisimani, kama mama yao aliyetumbukizwa akiwa hai lakini baadaye akafikwa na mauti.

Hata hivyo mshitakiwa huyo akiwa katika chumba cha mahakama kilichofurika watu hakutakiwa kujibu lolote, kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka kisheria kusikiliza shauri hilo ambalo litasikilizwa katika Mahakama Kuu.

Mwendesha Mashtaka, Mkaguzi wa Polisi, Ally Bwijo aliieleza mahakama hiyo kuwa mshitakiwa alitenda ukatili huo Aprili 6, mwaka huu saa 11:30 alfajiri ambapo aliwaua watoto wake hao wawili kisha miili yao na mama yao akiwa hai wakatumbukizwa katika kisima cha maji kijijini Majimoto.
Ilidaiwa pia kuwa mama huyo licha ya kuopolewa akiwa hai na kukimbizwa katika Kituo cha Afya kijiji Mamba, alifariki dunia Aprili 7, mwaka huu katika Hospitali ya Wilaya ya Mpanda alikohamishiwa kwa matibabu.

No comments:

Post a Comment