Monday, April 8, 2013

Madiwani Mpanda waandamana, wamkataa mkurugenzi mtendaji


MADIWANI wa Halmashauri ya Mji wa Mpanda mkoani Katavi wameandamana hadi ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Joseph Mchina wakitaka aondoke.

Madiwani hao wakiongozwa na Mbunge wa Mpanda Mjini, Said Arfi (Chadema) na Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo kabla ya kuanza maandamano hayo walikutana karibu na eneo la Shule ya Msingi Kashato.

Madiwani hao walipingana na umamuzi wa Mchina wa kuahirisha kikao cha Baraza la Madiwani kilichokuwa kifanyike jana, bila kutoa sababu za msingi.

Tuhuma alizotupiwa Mchina na madiwani hao ni pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo kutokuwa na ofisi hali inayomsababishia afanyie shughuli kwa kuomba chumba cha darasa shuleni.

Pia anadaiwa kuwa na tabia ya kuwagonganisha madiwani na watumishi na madiwani.

Tuhuma nyingine ni matumizi mabaya ya fedha na kukwepa kuitisha vikao vya sheria vikiwamo vya baraza la madiwani.

Akizungumzia msimamo huo wa madiwani, Arfi alidai kuwa kama Mchina yupo kwa maslahi ya watu fulani basi wamchukue wao na wakae naye ofisini kwao.

“Kama ni kisu sasa kimefika kwenye mnofu nikiwa na maana kuwa hatuko tayari kufanya tena kazi na Mchina (Mkurugenzi Mtendaji),” alisisitiza mbunge huyo.

No comments:

Post a Comment